Home » Kenya Power, Wasimamizi Wa Shirika La Reli Kukabiliana Na Wabunge Kuhusu Ukaguzi

Kenya Power, Wasimamizi Wa Shirika La Reli Kukabiliana Na Wabunge Kuhusu Ukaguzi

Wasimamizi wa kampuni ya Kenya Power watakabiliana na wabunge leo hii Jumanne kuhusu maswali kadhaa ya ukaguzi yaliyotolewa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Nancy Gathungu kwenye ripoti yake ya mwaka uliomalizika Juni 2021.

 

Kulingana na ripoti hiyo, mikataba yenye utata ya ununuzi wa kawi (PPA’s) ni miongoni mwa masuala muhimu ambayo yatachunguzwa na Kamati ya Bunge ya Kitaifa ya Uwekezaji wa Umma kuhusu Masuala ya Biashara na Kawi, inayoongozwa na Mbunge wa Pokot Kusini David Pkosing.

 

Gathungu alidokeza kuwa PPA’s huchangia asilimia 52 ya gharama ya uendeshaji ya kampuni.

 

Gathungu aliendelea kusema kuwa usimamizi wa Kenya Power ulionyesha kuwa mipango ilikuwa inaendelea kuoanisha tarehe za utendakazi wa kibiashara za PPAs na mahitaji ya kampuni ya muda wa kati, ili kwamba hakutakuwa na uzalishaji wa ziada wa umeme.

 

Pia timu ya Kenya Power inayosubiriwa ni suala la gharama ya kulinganisha ya kawi iliyonunuliwa kutoka kwa Kampuni ya Kuzalisha Umeme ya Kenya (KenGen) na Wazalishaji Huru wa Nishati (IPPs)

 

Aidha Gathungu alibainisha katika ripoti yake kwamba inagharimu Kenya Power wastani wa Sh5.3 kwa KWh kununua umeme kutoka KenGen na wastani wa Sh15.3 kwa kila KWh ya umeme kuzinunua kutoka kwa IPPs.

 

Wabunge hao pia watakuwa wakitafuta maelezo kutoka kwa Kenya Power kuhusu ni kwa nini malipo ya ununuzi wa umeme yalionyesha kuwa sehemu ya malipo ya uwezo wa nishati inayolipwa kwa IPPs mara zote ilikuwa kubwa kuliko gharama ya nishati halisi inayotolewa, kama mkaguzi mkuu alivyobainisha katika ripoti yake.

 

Zaidi ya hayo, timu ya Kenya Power inatarajiwa kueleza tofauti ya hasara ya Gigawati saa 2,899 (GWh) au asilimia 23.95 ya uniti za umeme ilizonunua.

 

Shirika la Reli la Kenya, kwa upande wake, litaelezea fidia ya Sh1 bilioni ya ardhi, iliyolipwa wakati wa awamu ya kwanza ya ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) lakini ambayo haijaungwa mkono na nyaraka zozote.

 

Katika ripoti yake, Gathungu anasema orodha ya wanufaika, nakala za vitambulisho vya kitaifa, vyeti vya nambari ya utambulisho wa kibinafsi (PIN) na waliosalimisha hati miliki kutoka kwa Tume ya Kitaifa ya Ardhi hazikutolewa kwa ukaguzi.

 

Pia linalosubiriwa na timu ya Shirika la Reli la Kenya ni suala la malipo ya ziada ya Sh8.9 milioni yaliyotolewa kwa watu kadhaa kufuatia ujenzi wa SGR.

About The Author

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

error: Content is protected !!