Rais Ruto Kuhutubia Mkutano Afrika Kusini

Rais William Ruto ameanza ziara ya siku mbili katika taifa la Afrika Kusini ili kuhutubia Mkutano wa Tatu wa Wabunge wa Afrika nzima kuhusu Sera na Usawa wa Hali ya Hewa.
Katika ziara hiyo, Msemaji wa Ikulu Hussein Mohamed amesema Rais Ruto atahutubia mkutano huo kwa wadhifa wake kama Mwenyekiti wa Kamati ya Wakuu wa Nchi na Serikali za Afrika kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (CAHOSCC).
Matokeo ya Mkutano huo, pamoja na ajenda zinazohusiana na biashara, yataingia katika Mkutano ujao wa Utekelezaji wa Hali ya Hewa wa Afrika utakaofanyika Nairobi, Kenya kuanzia tarehe 4 hadi 6 Septemba 2023.
Mkutano wa Kilele wa Nairobi utakuwa muhimu katika kuchagiza msimamo thabiti wa Afrika juu ya kushughulikia mabadiliko ya hali ya hewa, na kulisukuma bara la Afrika kutoka katika hali mbaya ya hewa hadi kuwa mshiriki hai katika suluhu za mabadiliko ya tabianchi.
Juhudi hizi za pamoja zitaendelezwa na kuwasilishwa katika vikao vya kimataifa vijavyo kama vile Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa na COP-28.