Home » Mhubiri Paul Mackenzie Kuzuiliwe Zaidi

Mkurugenzi wa Mashtaka wa Umma Noordin Haji amepata maagizo mapya ya kuendelea kumzuilia Mhubiri wa dhehebu lenye utata Paul Mackenzie ili kutoa muda wa kukamilisha uchunguzi.

 

Haya yanajiri baada ya DPP Haji kuzuru maeneo ya makaburi ya umati ya Shakahola yanayohusishwa na Mhubiri aliyekabiliwa na mzozo ambapo miili 17 iligunduliwa Jumanne na kufanya idadi hiyo kufikia 90.

 

Watu wanane pia waliokolewa na kuwafikisha watu 34 ambao hadi sasa wameokolewa wakiwa hai.

 

Uamuzi wa kupata maagizo hayo mapya umekuja baada ya uchunguzi wa awali kubainisha kuwa Mackenzie na wafuasi wake 14 wanaweza kuwa walikuwa wakiendeleza imani potovu kwa madhumuni ya kuwezesha vurugu zenye misingi ya kiitikadi ili kuendeleza mabadiliko ya kisiasa, kidini au kijamii.

 

Akibainisha kuwa upelelezi bado unaendelea, Haji alisema uamuzi wa kuwafungulia mashtaka washukiwa hao utatokana na ushahidi mzima.

 

Aidha, upande wa mashtaka umewaagiza maafisa wa upelelezi kubaini mali za watuhumiwa ili waweze kuhifadhi na kutaifisha kwa mujibu wa sheria.

 

Alisisitiza dhamira yake ya kukuza haki za binadamu na kutoa wito kwa watu binafsi na mashirika yote kufanya kazi pamoja ili kuunda jamii yenye amani na usawa kwa wote.

About The Author

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

error: Content is protected !!